UHURU WA MWANAHABARI UKO WAPI?



Tangu kale katika kisomo changu nimekuwa nikielezwa kuwa kuna uhuru wa mwanahabari, nikaelezwa pia juu ya uwepo wa taasisi mbalimbali za kupigania haki za mwanahabari pamoja na binadamu ikiwemo taasisi ya haki za binadamu.
Nilikuwa mwenye Imani kubwa na taaluma yangu, nikiamini kuwa ni imara na yenye kuheshimika kama taaluma nyingine nchini na duniani kote lakini leo hii nimetambua kuwa si hivyo bali ni maneno tuu.
Tazama leo hii, taaluma ya mwanahabari imepoteza heshima yake na kufananishwa na taaluma ya waarifu ambayo imejaa uadui mkubwa na polisi huku virungu vikiwa ni sehemu ya mawasiliano ya pande hizo mbili. Kibaya zaidi ni pale ambapo taaluma hii huitwa taaluma ya uchochezi na vurugu.
Naam twatambua kuwa wanahabari wengi katika jamii yetu ya Tanzania wamekuwa wakikutwa na mikasa kadha wa kadha wakiwa katika harakati zao za kukusanya habari ndani na nje ya nchi yetu. Mikasa mingine ikilihusisha jeshi la polisi na wengine kujeruhiwa pasipo julikana nani kamtendea hivyo.
Tazama hivi majuzi kabla ya marudio ya uchaguzi wa Zanzibar, mwanadada kutoka idhaya ya kiswahili ya DW, Salama Saidi, alipotea katika mazingira ya kutatanisha na hivyo kuzua maswali mengi kwa wanahabari wetu juu ya uzima wake. Kitendo kilicho-lazimu jukwaa la habari kutoa tamko la kulaani kitendo hicho pamoja na kuliomba jeshi la polisi kuingilia katika kumtafuta mwanamama huyo.
Kwa uwakika kupitia hiyo mikasa, tunaona ni jinsi gani maadhimio ya taasisi mbalimbali za kumlinda mwanahabari na taaluma yake zinavyokiukwa lakini pia katiba ya sasa inavyopindishwa kwa kumyima mwanahabari haki yake ya msingi ya kukusanya na kusambaza habari kwa jamii yake.
Sehemu ya 18 ya katiba ya Tanzania inabainisha kuwa kila mtu-
(a)   Anao uhuru wa kuwa na maoni na kueleza fikra zake;
(b)   Anayo haki ya kutafuta, kupokea na kutoa habari bila ya kujali mipaka ya nchi;
(c)    Anao uhuru wa kufanya mawasiliano na haki ya kutoingiliwa katika mawasiliano yake, na
(d)   Anayo haki ya kupewa taarifa wakati wote kuhusu matukio mbalimbali muhimu kwa maisha na shughuli za wananchi na pia kuhusu masuala muhimu kwa jamii.
Hakika msomaji umejionea katiba ya nchi inavyosema lakini mikasa kwa wanahabari haiishi kila kukicha.
Nina Imani ndugu msomaji unatambua juu ya mkasa wa kifo cha ndugu yetu Daudi Mwangosi ambaye alikuwa ni mwanahabari wa Channel ten, ambapo kifo chake kilimkuta katika harakati za kutafuta habari lakini pia tunakumbuka kitendo alichofanyiwa Saidi Kubenea cha kumwagiwa tindi kali mwilini.
Si hayati Daudi Mwangosi na Saidi Kubenea waliokutwa na mikasa hiyo pekee bali tunatambua kuwa kuna wenginie wengi waliokutwa na mikasa tofauti tofauti ikiwemo ndugu yetu Jumbe Ismailly, Mwinyi Sadala, Tegambwage na waandishi wengine wengi.
Ni dhahiri kuwa taaluma hii imepoteza uhai wake kutokana na mikasa ambayo imekuwa ikiwakumba wanahabari kila kukicha, na hivyo kupelekea wanahabari kukosa uwaminifu kwa serikali na vyombo vyake vya ulinzi ambavyo vimekuwa vikisihii wanahabari waungane nao katika ujenzi wa jamii yetu.
Jambo ambalo limesababisha wanahabari wengi kusahau nini taaluma yao inapawapasa kufanya kwa hofu ya kupata majeraha na kulinda uhai wao kwani hata taaluma na sheria zilizotungwa nazo si kwa ajili ya kumtetea mwanahabari bali zimepindishwa na kuwa msumeno mkali dhidi ya wanahabari.
Swala la miiko ya habari, tuliyofundishwa pindi tulipokuwa katika mafunzo ya uwandishi bora katika taaluma yetu ya uwanahabari imekuwa ikitupiliwa mbali leo hii na kulazimu wanahabari walio wengi kusimama na kutukuza yale serikali inafanya hata kama pale serikali inakosea na inahitaji kukoselewa ili ijirkebishe.
Ni waandishi kadhaa leo hii wamekuwa tayari kuikosoa serikali pindi ikoseapo huku wengi wakiwa wemejengwa kwa misingi ya kufuata matakwa yao ya kiuchumi au ya wamiliki wao, wamiliki hao wengi wamekuwa wakitulazimu wanahabari tuwe kasuku kwa kurudia yale washika dola wanayoyataka kwa kuhofu na kulinda uhai wa chombo husika.
Hakika swali juu ya uhuru wa mwanahabari katika nchi hii ni swali ambalo kila mwanahabari anapaswa kujiuliza na alitambue, japo ni dhahiri kuwa uhuru wa taaluma hii ni wa wastani sana tangu kipindi cha mkoloni hadi sasa.
Adhabu zilizopo juu ya mwanahabari ni kubwa kuliko ule ulinzi aliopewa juu yake katika shughuli zake za kukusanya na kusambaza habari juu ya jamii yake. Jambo linalomjaza hofu na kumlazimu kushindwa kufanya kazi katika uwaridi mkubwa.
Imani yangu ipo juu ya Mheshimiwa Raisi Dokta John Pombe Magufuli kupitia kauli aliyoitoa kuwa hatatuacha wanahabari kwani atatuangalia na kutusaidia, japo sidhani kuwa jicho lake litajikita tuu katika kufungia magazeti ila kuongeza uhuru wa habari na hili litawezekana kwa kutunga sheria imara za kulinda wanahabari wote ndani ya nchi yetu Tanzania.
Lakini si kwa kutunga sheria na vifungu kandamizi ambavyo vitamzuia mwanahabari ajikite katika katika ukweli bali akjikita katika siasa ambayo imejazwa maigizo na utata mtupu. Itakuwa ni vyema vifungu hivyo vimlinde mwanahabari katika nyanja zake zote za taaluma yake ikiwemo ukusanyaji na usamabazaji.
Makala hii imeandaliwa na mwanafunzi wa mwaka wa pili katika Shule Kuu ya Uwandishi wa Habari na Mawasiliano kwa Umma. Kwa mawasiliano zaidi
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment

0 comments:

Post a Comment